Home » » HII NDO BARUA YA MH.MBATIA KWA RAISI

HII NDO BARUA YA MH.MBATIA KWA RAISI

Written By shebby on Tuesday, March 5, 2013 | 12:29 AM

Rais Dk. Jakaya Mrisho Kikwete.
HALI ya elimu nchini hairidhishi na inatisha. Kutokana na kutambua umuhimu wake,  nimemwandikie barua Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete, nikitoa mapendekezo ambayo mimi na wanachama wenzangu wa NCCR-Mageuzi, tumeona yanaweza kuleta tiba kama si kupunguza tatizo.
Mhe. Rais, katika muktadha wa mapendekezo tunayoyaleta kwako tunazingatia  masuala ya kitaifa yafuatayo;
 (i) Tangu taifa letu lipate uhuru wake mwaka 1961 (kwa Tanganyika) na mwaka 1964 (Mapinduzi ya Zanzibar) tulitambua umuhimu wa kufuta ujinga, kwa kuelimisha wananchi ili tujiletee maendeleo. Ingawa hadi sasa kazi kubwa imefanyika katika kukuza elimu hapa nchini, bado hatujafika katika hali ya kuwa na taifa ambalo karibu kila raia mwenye umri stahiki anajua kusoma na kuandika.
 (ii)  Katika Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025, tunataja pamoja na mambo mengine kwamba, ifikapo mwaka 2025 tuwe tumejenga taifa la watu walioelimika kwa upeo wa juu katika nyanja mbalimbali.
 (iii) Tanzania ni miongoni mwa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, ambao una malengo nane ya milenia; lengo la pili likiwa ni upatikanaji wa elimu bora kwa wote.
(iv) Ifikapo mwaka 2015 (takriban miaka miwili toka sasa) tutalazimika kama taifa kupima utekelezaji wa malengo hayo ili kuendana na viwango vya kimataifa.
Mheshimiwa Rais,
Wakati tukikabiliwa na malengo hayo ya Kitaifa, kwa muda mrefu kumekuwepo na viashiria vingi vinavyoonesha kwamba ubora wa elimu itolewayo hapa nchini katika ngazi zote hauridhishi. Viashiria hivyo ni;
(a) Matokeo ya hivi karibuni ya mitihani ya kidato cha nne nchini yanaonesha kuendelea kushuka kwa viwango vya ufaulu wa wanafunzi.
(b) Taarifa mbalimbali zimeonesha kuwa wanafunzi wengi wanaohitimu elimu ya msingi na kujiunga na elimu ya sekondari wana uwezo mdogo katika stadi za kusoma na kuandika na wengine hawawezi kabisa kusoma wala kuandika.
(c) Shule nyingi za umma zinakuwa na matokeo mabaya ya mitihani ikilinganishwa na zile zinazomilikiwa na watu binafsi au mashirika yasiyo ya kiserikali.
(d) Tanzania inashika nafasi ya ngapi kielimu katika Afrika Mashariki?

Athari za udhaifu wa elimu kwa taifa

Mheshimiwa Rais,
Athari za udhaifu katika elimu itolewayo nchini zinajidhihirisha katika sura mbalimbali, miongoni mwazo ni hizi zifuatazo;
i. Kumong’onyoka kwa mila, desturi na utamaduni wa jamii ya Watanzania.
ii. Kuporomoka kwa uadilifu miongoni mwa watumishi wa umma na kada nyinginezo na hivyo ongezeko la ufisadi na rushwa.
iii. Kuporomoka kwa uwajibikaji.
iv. Kuporomoka kwa kiwango cha utii wa  sheria na kanuni mbalimbali.
v. Kutothamini rasilimali za taifa.
vi. Tabia ya Watanzania wengi kutothamini matumizi ya muda.
vii. Kupungua kwa uzalendo kwa baadhi ya wananchi.
viii. Kutojiamini kwa Watanzania wanaohitimu elimu katika ngazi mbalimbali.
ix. Ukosefu wa nidhamu ya matumizi ya tekinolojia ya habari na mawasiliano (Tehama), mfano matumizi ya simu nururu (mobile phones) na mitandao ya kijamii wakati wa kazi bila kuzingatia umakini kwenye kazi mtu anoyafanya.

Mheshimiwa Rais,
Vilevile udhaifu ulioko katika elimu ndiyo hatimaye husababisha matatizo yafuatayo;
i. Kuporomoka kwa viwango vya huduma zitolewazo katika sekta mbalimbali.
ii. Kuporomoka kwa viwango na ubora wa bidhaa, majengo na miundombinu.
iii. Kuporomoka kwa viwango vya uzalishaji wa bidhaa mashambani na viwandani.
iv. Uharibifu na uchafuzi wa mazingira.
v. Udhaifu katika kukabiliana na majanga mbalimbali kama vile mafuriko na tetemeko la ardhi.
vi. Udhaifu katika kuzuia na kudhibiti ajali zinazoweza kuzuilika, kama vile ajali za vyombo vya usafiri, moto na  milipuko ya silaha.
vii. Udhaifu katika kukabiliana na hatari za kiafya kwa binadamu na wanyama zitokanazo na uchimbaji migodini na usafirishaji  au uhifadhi wa kemikali.
viii. Migomo ya watumishi wa umma pamoja na makundi ya kijamii inayojitokeza katika ngazi mbalimbali, vurugu na migogoro katika jamii.
Chimbuko la tatizo na hatua tulizojaribu Kuchukua

Mheshimiwa Rais,
Baada ya tafakuri na utafiti wa muda mrefu sasa, NCCR – Mageuzi tumebaini kuwa, elimu ya Tanzania imedidimia zaidi kupitia mamlaka zinazoisimamia. Mifano ya matatizo yanayotokana na mamlaka husika ni kama ifuatavyo;
(a) Kukosekana kwa mitaala ya elimu nchini, ilhali ipo taasisi husika kwa ajili ya utengenezaji mitaala. Hili ni tatizo kubwa mno linalowafanya walimu wafundishe wanafunzi bila kuwa na mwongozo wa pamoja na hivyo kuifanya elimu itolewayo itegemee ufahamu wa mwalimu mmoja mmoja.
(b) Ukosefu wa umakini katika kuandaa vitabu vya kiada na ziada kwa ajili ya matumizi ya shule mbalimbali, ilhali ipo taasisi inayoidhinisha matumizi ya vitabu mashuleni. Vitabu vilivyoandaliwa na vinavyotumika kwa sasa vina upungufu mkubwa ya weledi na muongozo.
(c) Mfumo wa mitihani kukosa mwongozo wa kueleweka, japo nchi inacho chombo maalum kwa ajili ya mitihani ya kitaifa. Imefikia hatua wanafunzi wanapimwa uelewa wao kwa maswali ya kuchagua majibu na kubahatisha. Japokuwa mfumo huo ni mzuri kwa usaili na kurahisisha matokeo kutoka kwa wakati, una uwezo mdogo wa kupima uelewa wa mwanafunzi.
(d) Wingi wa masomo kwa wanafunzi wa umri mdogo, wanafunzi wa elimu ya awali wamewekewa kiwango kikubwa cha mzigo wa masomo bila kujali uwezo wao wa ufahamu na kuzingatia umri pamoja na kwamba wapo wataalam nchini wa mitaala na mafunzo.
Kadhalika, darasa la kwanza (elimu ya msingi) wanaanza kwa kufundishwa masomo manane. Hii inashusha uwezo wa mwanafunzi kutambua mambo ya msingi na hatimaye anajikuta hatambui chochote.
(e) Kukosekana kwa waalimu wenye weledi kwenye baadhi ya masomo katika shule za umma, licha ya kwamba nchi inavyo vyuo mbalimbali vya mafunzo ya ualimu.
(f) Mazingira duni ya kazi yameshusha kwa kiwango kikubwa ari ya kufanya kazi miongoni mwa walimu.
(g) Mfumo uliopo umeshindwa kufanya ufuatiliaji na ubaini wa matatizo ya elimu katika ngazi mbalimbali za elimu kwa nchi nzima, licha ya kwamba taifa linao wakaguzi wa elimu.

Mheshimiwa Rais,
Tunatambua tatizo lililopo na tumejaribu kupitia kwa wawakilishi wetu katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kulishirikisha Bunge katika kutafuta ufumbuzi wa tatizo hili. Bahati mbaya jitihada zetu kupitia huko hazikufanikiwa.

Itaendelea toleo lijalo.
NA JAMES MBATIA
Share this article :

Post a Comment

 
thanx to : my family | bongoclan | shebby.c
Copyright © 2011. BONGODASH - All Rights Reserved
imetengenezwa na blogdesinerimepigwa chapa na mchakato
Proudly powered by Blogger