Home » » HII NI HISTORIA KWA MPAMBANO WA WANAUME HARISI VS FAMILY NDANI YA DAR LIVE

HII NI HISTORIA KWA MPAMBANO WA WANAUME HARISI VS FAMILY NDANI YA DAR LIVE

Written By shebby on Wednesday, April 3, 2013 | 11:02 PM

Na Mwandishi Wetu
MUZIKI mzuri ulipigwa, watu wazuri wakashangilia burudani kali, wakaikubali shoo ya Wanaume Family huku wengine wakimkubali Juma Kassim ‘Nature’ na kundi zima la Wanaume Halisi, ilikuwa ni bonge la historia.
Ulikuwa ni mpambano wa kukata na shoka, uliopigwa Jumapili iliyopita katika Ukumbi wa Dar Live, Mbagala Zakhem, jijini Dar ambapo mashabiki walionesha kuyakubali makundi yote mawili kwa kufanya shoo kali pamoja na wasanii wengine waliosindikiza.
Asubuhi hadi jioni, watoto walifurahia michezo mbalimbali iliyopo ndani ya ukumbi huo likiwemo bembea jipya ambalo lilizinduliwa rasmi katika Sikukuu ya Pasaka.
Giza lilipoingia watu wazima walianza kupashwa moto na Malkia wa Mipasho Bongo, Khadija Kopa na bendi nzima ya Tanzania One Theatre ambaye alishusha sebene baab’kubwa na kuwafanya mashabiki waziimbe nyimbo zake, mwanzo mwisho.
Kuelekea kwenye mpambano, Mic ilikabidhiwa kwa Ispector Haroun ‘Babu’ ambaye aliamsha hisia za shoo kwa kugonga nyimbo zake kali zilizobamba kitambo ikiwemo Asali wa Moyo (remix) ambayo iliitikiwa kwa shangwe kubwa na mashabiki waliokuwa wakidansi kwenye eneo la kuchezea.
Mara baada ya Babu kuamsha mzuka wa burudani, Wanaume Halisi ndiyo walikuwa wa kwanza kutupa karata yao ya kwanza kwa kuwapandisha baadhi ya wasanii wake wachanga na kupiga shoo kali iliyopata shangwe la kutosha.
Kama ilivyokuwa kwa Wanaume Halisi, Wanaume Family nao katika raundi ya kwanza waliwatanguliza wasanii wake wasio na majina makubwa ambao pia walishangiliwa kwa sana.
Baada ya raundi hiyo ya kwanza, ulikuwa ni muda wa mapumziko ambapo legend wa Hip Hop Bongo, Profesa Jay aliutumia vilivyo kushusha shoo classic ambayo ilinakshiwa na DJ mkongwe Bongo, JD aliyesimama kwenye moja na mbili huku akiwa miongoni mwa majaji wa mpambano huo.
Baada ya mapumziko, raundi ya mashambulizi ndiyo ilifuata ambapo Wanaume Family walikipandisha kikosi kizima cha maangamizi kilichoongozwa na Chegge na Temba na umati mzima uliofurika ukimbini ulipagawa na kucheza nyimbo zao kali kama Kichwa Kinauma, Dar Mpaka Moro na nyinginezo.
Pazia la burudani lilikamilishwa na Wanaume Halisi ambao walipiga nyimbo zao kali ikiwemo Ndege Tunduni na umati ulilipuka kwa furaha haswa wakimshangilia Nature.
Hadi mwisho wa shoo, makundi yote yalifanya vizuri. Wanaume Halisi walionekana kupendwa haswa kwa mashabiki wengi kumkubali Nature, lakini Wanume Family walikubalika zaidi kwa kuangusha shoo kali iliyoteka hisia za watu wengi jukwaani hivyo mashabiki kuugawanya ushindi kwa makundi yote mawili kulingana na vigezo vyao.
Historia inaonesha mara ya mwisho makundi hayo yalipokutana katika Ukumbi wa Diamond Jubilee mwaka 2008, kulikuwapo na vurugu za hapa na pale lakini asikwambie mtu, shoo ya Dar Live, mwaka huu ilitawaliwa na amani na mashabiki waliinjoi shoo kistaarabu mwanzo hadi mwisho. Mpango mzima ulisimamiwa na udhamini wa Serengeti Premium Legar, Pepsi na Vodacom.
Share this article :

Post a Comment

 
thanx to : my family | bongoclan | shebby.c
Copyright © 2011. BONGODASH - All Rights Reserved
imetengenezwa na blogdesinerimepigwa chapa na mchakato
Proudly powered by Blogger