Home » » YANGA YATAKA UBINGWA J TANO

YANGA YATAKA UBINGWA J TANO

Written By shebby on Tuesday, April 16, 2013 | 3:33 AM

Kocha wa Yanga, Ernie Brandts, amesema kwamba endapo timu yake itashinda mechi yake ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara itakayofanyika Jumatano jijini Tanga tayari itakuwa imejihakikishia kutwaa ubingwa wa ligi hiyo.
 
Brandts alisema kuwa baada ya ushindi wao wa juzi wa mabao 3-0 dhidi ya JKT Oljoro kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, haoni kikwazo cha kutwaa ubingwa ikiwa watapata pointi nyingine tatu ugenini jijini Tanga.
 
Mholanzi huyo alisema kuwa kikosi chake kimeimarika zaidi na kiwango cha juu walichokionyesha katika mechi yao dhidi ya Oljoro kimempa matumaini makubwa ya kutwaa ubingwa kabla ya mechi yao ya mwisho watakayovaana na mahasimu wao wa jadi, Simba.
 
Kocha huyo alisema kuwa anataka kuona Jumatano wanashinda ugenini na kujiweka katika nafasi nzuri kabla ya kukutana na watani zao wa jadi, Simba katika mechi itakayofunga msimu wa ligi.
 
Aliwapongeza pia wachezaji wake kwa kutumia vyema nafasi walizopata na kuhitimisha mwendo wa kusuasua wa kupachika mabao ulioonekana katika mechi zao za hivi karibuni, akisema kuwa hayo ni matunda ya kazi kubwa waliyoifanya kwa wiki mbili kabla ya mechi ya juzi.
 
''Wiki mbili zote nilikuwa nikiwapa mazoezi ya kufunga, tena kila mchezaji... mwishowe magoli yamepatikana. Nitaendelea kuwapa mbinu zaidi wachezaji wangu,'' alisema kocha huyo.
 
Aliongeza kuwa ushindi wa keshokutwa Jumatano utaondoa hofu dhidi ya Azam ambao wako katika nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi.
 
Alisema kwamba hali za wachezaji wake wawili walioumia juzi, Didier Kavumbagu na Juma Abdul zitajulikana leo kama watasafiri kesho kuelekea Tanga kuwakabili wenyeji wao JKT Mgambo.
 
Yanga ndiyo vinara wa ligi ambao sasa wamefikisha pointi 52, wakati watani zao Simba wakiwa wameshapoteza nafasi ya kutetea ubingwa huku Azam ambao walitoka sare ya 2-2 katika mechi yao dhidi ya Simba jana wakiwafuatia katika nafasi ya pili baada ya kufikisha pointi 47.
CHANZO: NIPASHE
Share this article :

Post a Comment

 
thanx to : my family | bongoclan | shebby.c
Copyright © 2011. BONGODASH - All Rights Reserved
imetengenezwa na blogdesinerimepigwa chapa na mchakato
Proudly powered by Blogger